3. Kwaresima,Toba na “unafiki”

Toba na “unafiki”
Katika Enjili ya Misa ya Jumatano ya Majivu (Mt. 6: 1-6, 16-18), Yesu anatamka mara tatu neno hili: “wanafiki”:
“Basi wewe utoapo sadaka, usipige panda mbele yako, kama wanafiki wafanyavyo katika masinagogi na njiani, ili watukuzwe na watu” (Mt. 6:2).
“Tena msalipo, msiwe kama wanafiki: kwa maana wao wapenda kusali hali wamesimama katika masinagogi na katika pembe za njia, ili waonekane na watu” (Mt. 6:5).
“Tena mfungapo, msiwe kama wanafiki wenye uso wa kukunjamana; maana hujiumbua nyuso zao, ili waonekane na watu kuwa wanafunga” (Mt. 6: 16) .
Ndani ya Biblia maneno “unafiki”, “mnafiki” na “wanafiki” yanarudiwa mara 29 hasa ndani ya Agano Jipya:
 YbS 1:29; 28:13; 32:15;
 Mt. 6:2,5,16; 7:5; 15:7; 22:18; 23:12,13,15,23,25,27,29; 23:28; 24:51
 Mk. 7:6
 Lk. 6:42; 12:1,56; 20:44
 Rum. 12:9
 1Tim. 4:2
 2Tim. 1:5
 Yak. 3:17
 1 Pet. 2:1; 1:22
Tafsiri ya neno “mnafiki” ndani ya kamusi ni hali ya kutokuwa mkweli. Kivumishi “mnafiki” ni mtu anayesema kinyume na anavyotenda.
Fasili hii inatusaidia pia kuelewa maana ya “unafiki” katika Biblia, hasa Agano Jipya. Ni njia inayoweza kutumika na muumini ili aonekane mwema kwa nje au akiwa pamoja na wengine, ila moyoni mwake anawaza tofauti au asipoonekana na wengine anatenda kinyume na mwongozo wa imani yake. Mara nyingine huwa anafanya hivyo ili watu wasitambue mapungufu au ufisadi wake., au ili apate faida fulani, kwa mfano sifa, heshima...
Yesu anakemea vikali mfumo huu na pia watu wanaoutumia bila haya, hasa wale wanaotumia dini kwa matumizi yao binafsi tena mabaya. Tabia ya namna hiyo aliiona wazi kwa Waandishi na kwa Mafarisayo.

Nessun commento: